0
 MWENYEKITI WA WAFANYABIASHARA(TCCIA)MKOA WA MARA MR.GIBOGO AKIZUNGUMZA JAMBO
 MFANYABIASHARA MARTINI KOROGO AKICHANGIA KWENYE MGOMO WA WAFANYABIASHARA
 MKUU WA WA MKOA WQA MARA JOHN TUPA KUSHOTO AKITETA JAMBO NA MENEJA WA TRA BAADA YTA MGOMO WA WAFANYABIASHARA
 SEHEMU YA MADUKA YALIYOFUNGWA MJINI MUSOMA

WAFANYABIASHARA wa mjini Musoma wamegoma kufungua biashara zao katika maduka ya huduma mbalimbali wakidai kutokuelewa mfumo wa matumizi ya mashine za kieletroniki EFDs pamoja na watumishi wa  Mamlaka ya Mapato(TRA)kuwapa majibu yasiyo mazuri na kugoma kupokea vitabu vyao vya mauzo kwa ajili ya mahesabu hali iliyopelekea mkuu wa mkoa wa Mara pamoja na meneja wa TRA kukutana nao.

Katika mgomo huo ambao uliitikiwa na wafanyabiashara wote mjini hapa,walidai TRA wameshindwa kutoa elimu ya kutosha kwa wafanyabiashara kutokana na matumizi ya mashine hizo na kinachoonekana kwa sasa kuna mpango ambao unakusudiwa na watumishi wa TRA kuwabana zaidi baada ya kugoma kupokea vitabu vyao vya mauzo kwa ajili ya kukadiliwa kodi.

Katibu wa wafanyabiashara wadogo mjini Musoma Bugoro Marwa alisema wameanza kuona mapema manyanyaso kutoka kwa baadhi ya watumishi wa TRA kwa kushindwa kupokea vitabu vyao hivyo wameamua kuweka mgomo wa kutokufungua maduka ili wapewe muongozo mzuri na wafanye biashara zao kwa amani.

Alisema  baadhi ya wafanyabiashara walikwenda katika ofisi za TRA lakini walikutana na manyanyaso kutoka kwa watumishi wake na kuona ni vyema kuchukua maamuzi ya kugoma kufungua biashara zao ili waweze kupata ufumbuzi juu ya kile ambacho kimeanza kuonekana baada ya kugoma kupokelewa vitabu vyao vya mahesabu.

Bugoro alisema hakuna mfanyabiashara ambaye anaweza kugomea kulipa kodi kwa kuwa hakuna Serikali inayoweza kuendeshwa bila kodi lakini mfumo unaofanywa wa ukusanyaji kodi sio rafiki kwa wafanyabiashara na unazidi kuwarudisha nyuma.

Alisema licha ya kuhusiana na  suala la mashine za EFDs katika mji wa Musoma kumekuwa hakuna mahusiano mazuri kati ya watumishi wa TRA na wafanyabiashara katika ukusanyaji wa kodi hali iliyopelekea wafanyabiasha wengi kuhama Musoma na kwenda kufanya biashara katika miji mingine na kuuacha mji wa Musoma ukiwa na maendeleo duni.

“Hapa lazima tuelezane ukweli,wafanyabiashara wengi wa mji wa Musoma wamehama na kwenda miji mingine kutokana na manyanyaso ambayo wamekuwa wakifanyiwa na watumishi wa TRA na kufanya mji huu ukiwa nyuma kimaendeleo kila kukicha,”alisema  Bugoro.

Mmoja wa wafanyabiashara hao aliyejitambulisha kwa jina la Beatrece Libamba alisema wakina wanawake wajasiliamali ndio wanaoumizwa sana na mfumo wa ukusanyaji kodi wa TRA kutokana na kuchukua mikopo katika taasisi za fedha na kupelekea kushindwa kurejesha kutokana na makusanyo ya kodi kutoka TRA.

Meneja wa Mamlaka ya Mapato(TRA) mkoa wa Mara Joseph Karinga alisema bado wanaendelea kupokea vitabu vya wafanyabiashara kwa hesabu za mwezi januari na kama kuna mtumishi ambaye aligoma kupokea vitabu wampelekee ofisi kwake ili hatua za kinidhamu ziweze kuchukuliwa.

Akizungumza na wafanyabiashara hao baada ya kukutana nao kutokana na mgomo huo.mkuu wa mkoa wa Mara John Tupa alisema ni vyema wafanyabiashara kabla ya kuchukua uamuzi wa kugoma wangemuona na kukaa pamoja ili kuweza kuzungumza na kuona kero zinazowakabili kutoka kwa watumishi wa TRA.

Alisema ni vyema kama kuna suala lolote linalo wakwanza wafanyabiashara ofisi yake ipo wazi na yupo tayari kukutana nao na kama itaonekana mtumishi yoyote ambaye afuati maadili ya kazi atachukuliwa hatua na mtu yoyote asisite kutoa taarifa kwenye vyombo vinavyohusika.

Tupa alisema kutokana na nafasi yake ya mkuu wa mkoa hawezi kuzungumzia suala la mashine za EFDs kwa kuwa tayari limeshazungumzwa na Seriksali inalo hivyo anaamini linafanyiwa kazi na kudai suala la kufanya mgomo linawaathiri wengi na kusema yupo tayari kukutana nao ili kuweka meza ya mazungumzo na kuyafikisha mahala husika.

Kufuatia hali hiyo baadhi ya wananchi wa mji wa Musoma wameiomba Serikali kuangalia suala la wafanyabiashara na mashine za EFDs kwa kuwa mgomo wa wafanyabiashara unakwamisha huduma mbalimbali ikiwemo hata maduka ya dawa kufungwa kutokana na mgomo huo.

Walisema kila mahala hapa nchini wafanyabiashara wamekuwa wakilalamikia mashine hizo na kuiomba Serikali kutazama upya suala hilo kwa kuwa wanaoathirika ni pamoja na wananchi ambao wamekuwa wakishindwa kupata huduma kutokana na mgomo wa wafanyabiashara unaojitokeza mara kwa mara.

Post a Comment