0
MGOMBEA NAFASI YA MWENYEKITI WA CCM MKOA WA MARA CHRISTOPHER SANYA

Mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mara Christopher Sanya amemshukuru Mwenyekiti wa Chama hicho Taifa Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na wajumbe wote waliopitisha jina lake katika kuwania nafasi hiyo kwa kuwa wamemuamini na kuona anafaa kukiongoza Chama hicho.

Akizungumza na blogu hii mara baada ya kikao cha Kamati kuu ya Chama hicho kulitangaza jina lake kuwa mmoja wa wagombea wa nafasi hiyo katika Mkoa wa Mara,Sanya alisema kazi imebakia kwa wajumbe wa mkutano mkuu wa uchaguzi wa ambao ndio utakuwa na maamuzi ya mwisho ya kuamua ni kiongozi gani mwenye nia ya dhati katika kukifanya Chama cha Mapinduzi kuendelea kuongoza.

Alisema iwapo wajumbe wa mkutano wa uchaguzi watamuamini kama ambavyo ameaminiwa na vikao vya juu vya Chama atahakikisha anaondoa dhana ya makundi yaliyokuwa yamejengwa na viongozi wenye kupenda ubinafsi badala ya kuwaunganisha wanachama na kufanya kazi za Chama  

Sanya alisema ni muhimu kutolewa kwa elimu ya Chama kwa Wanachama ili kila mmoja aweze kuelewa umuhimu wake ndani ya Chama na kutekeleza majukumu yanayompasa katika kukitumikia na kujitambua.

Alisema wapo wagombea ambao wanaomba nafasi kwa ajili ya kutafuta majina na umaarufu na kushindwa kuzitumia kwa kuleta ufanisi na mabadiliko ndani ya Chama hicho na kufanya kuyumba kwa Wanachama huku wengine wakikimbilia katika vyama vya upinzani.

Aliongeza kuwa  ni vyema Mwanachama unapoomba nafasi ya uongozi kujiuliza nini utakifanyia Chama kuliko kuomba nafasi kwa kutafuta ufahamike na kuhudhuria vikao bila kuwa na mipango ya kujua namna ya kuongeza Wanachama na kuwajenga kiimani Wanachama wote ili kuepuka mkanganyiko.

Alisema ni muhimu kuendesha madarasa ya itikadi ili kuwafanya wanachama na viongozi wao kujua kwa nini akawa kiongozi ama mwachama kwa kufanya hivyo kila mwanachama atajitambua na kuwa na ujasili binafsi badala ya kusubiri asemewe kila wakati na kupoteza haki zake kichama.


Akizungumzia masuala ya kiuchumi  Sanya alisema kutokana na vitega uchumi vilivyopo ndani ya Chama hicho ataanzisha makampuni ya biashara ya ushindani kila Wilaya ya Mkoa wa Mara ili kila kada wa Chama hicho aweze kujipatia kipato na kuendesha maisha pamoja na kufanya kazi za Chama.    

Alidai kutokana na vitega uchumi hivyo atahakikisha anasimamia akiwa kama mwana uchumi ili kuleta mabadiliko ya kiuchumi ndani ya Chama cha Mapinduzi na kila mmoja aweze kuvutiwa na Chama hicho si kwa sera peke yake bali na kujiendesha kiuchumi.

Katika kuelekea Uchaguzi wa Selikari za mitaa Mwaka 2014 Sanya alisema iwapo wanachama watachagua viongozi wenye nia ya dhati ndani ya Chama hicho na kukuachana na wagombea watoa rushwa ili wapate uongozi  ndio itakuwa nafasi ya kufanya vizuri katika Uchaguzi huo na Uchaguzi mkuu wa Mwaka 2015.



Post a Comment