0

RAIS WA GHANA JOHN MAHAMA AKIAPISHWA



Chama kikuu cha upinzani nchini Ghana, kimesusia sherehe za kuapishwa kwa rais John Mahama kufuatia uchaguzi wa mwezi uliopita uliokumba na utata.

 Chama cha New Patriotic Party (NPP) kimedai Bwana Mahama alishinda uchaguzi huo kwa njia ya udanganyifu.

Matokeo rasmi yalimpa Bwana mahama ushindi wa asilimia 50.7, ya kura zote zilizopigwa, kiwango ambacho kinamfanya kuongoza duru ya pili ya uchaguzi dhidi ya mgombea wa chama cha NPP Nana Akufo-Addo, ambaye alipata 47.7%.

Kabla ya kuapishwa kwake rais Mahama alitoa wito kwa raia wa nchi hiyo kuwa watulivu na kuwa na umoja, ili kudumisha demokrasia yao ambayo kwa sasa inakisiwa ndiyo thabiti zaidi barani Afrika.

Bwana Mahama alikuwa makamu wa rais hadi kifo cha ghafla cha rais John Atta Mills mwezi Julai mwaka uliopita.
Tangu wakati huo amekuwa akihudumu kama kaimu rais wa nchi hiyo.

Katika hotuba yake, rais Mahama aliwaambia raia wa nchi hiyo kuwa hatapuuza maslahi yao na kuwa atafanya kila juhudi ili kuleta maendeleo.

''Ahadi nilizotoa, ndizo ahadi nitakazo timiza'' Alisema rais Mahama.

Siku ya Ijumaa wiki iliyopita rais huyo alitoa wito kwa wabunge wa nchi hiyo kushirikiana.

Maelfu ya wafuasi wa rais huyo walifurika bustani ya uhuru iliyoko katika mji mkuu wa nchi hiyo, Accra, kuhudhuria sherehe hiyo.
Marais kadhaa wa mataifa ya Kiafrika walihudhuria sherehe hiyo ikiwa ni pamoja na rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma na rais wa Nigeria Goodluck Jonathan.

        Chanzo BBC SWAHILI;

Post a Comment