0
 DAWATI ALILOKUWA AKIJISOMEA MWALIMU NYERERE
 ORODHA YA WANAFUNZI WALIOSOMA SHULE YA MSINGI MWISENGE
 MWALIMU MKUU WA SHULE YA MSINGI MWISENGE MWALIMU TAIRO
 JENGO ALILOKUWA AKIISHI MWALIMU WA MWALIMU NYERERE
 JENGO LILILOKARABATIWA
 OFISI YA WALIMU
OKTOBA 14, mwaka huu, taifa la Tanzania linaadhimisha Miaka 14 ya Kumbukumbu ya Kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius K. Nyerere aliyeaga dunia 0ktoba 14, 1999 katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas, jijini London, nchini Uingeleza alikokuwa amekwenda kupata matibabu.

Mazuri mengi yatazungumzwa kuhusiana na Mwalimu Nyerere lakini mimi nitajikita pale shule ya msingi Mwesenge  iliyopo Manispaa ya Musoma,shule ambayo Baba wa Taifa hili alitembea umbali wa kilometa 37 kutoka Kijijini Mwitongo Butiama kwenda kupata elimu ya msingi kwenye shule hii. 

Hii ni shule yenye historia kwani licha ya Mwalimu Nyerere kusoma kwenye shule hii wapo viongozi wengine waliopata kushika nafasi kubwa na wengine bado wana nafasi kubwa akiwemo Waziri Mkuu wa zamani na Mwenyekiti wa wa Tume ya mchkato wa kupata Katiba mpya Jaji Joseph Sinde Warioba.

Orodha ni ndefu ya viongozi waliokuwa wanafunzi wa shule hii ambayo inaelezwa licha ya Serikali kujitahidi kuweka mazingira mazuri ya shule kutokana na historia yake bado inakumbwa na matatizo lukuki ikiwemo kukosa matundu ya vyoo na kupelekea wanafunzi wa shule hiyo kukosa mahala pa kujisaidia!.

Licha ya viongozi hao nilioanza nao waliosoma kwenye shule hii,wengine waliosoma Hapa ni Bhoke Munanka huyu alipata kuwa Waziri katika Ofisi ya Rais wa awamu ya kwanza na kufanya kazi kwa karibu na Mwalimu.

Pia kuna majina ya Joseph Butiku aliyekuwa Katibu wa Rais Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ambaye kwa sasa yupo karibu na makumbusho ya Mwalimu,Richard Wambura aliyepata kuwa Balozi wa Tanzania katika Nchi mbalimbali naye amesoma Mwisenge.

Majina kama Mutaragara Chirangi aliyekuwa Katibu wa elimu,Selemani Kitundu na Oswrd Marwa waliopata kushika nafasi ya Mkuu wa mkoa wa Mara kwa vipindi tofauti wote wamesoma kwenye shule hii.

Kwa safu hiyo ya viongozi waliosoma Mwisenge shule ya msingi kuna kila sababu ya kusema ni shule ya kihistoria kwa Taifa hili inayopaswa kuenziwa kwa kuangalia changamoto zinazoikabili hili historia yake iendane na mazingira yake.

“Baadhi ya majengo hali yake ni nzuri kutokana na Serikali kuamua kuyakarabati ili kumuenzi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lakini mengine bado hayajakarabatiwa ni chakavu na nyumba wanazoishi walimu ni mbovu na haziendani na hadhi ya jina la shule hii.

“Ile nyumba unayoiona ndio aliyokuwa anaishi Mwalimu aliyekuwa anamfundisha muasisi wa Taifa hili pamoja na viongozi wengine waliopata kusoma kwenye shule hii ni budi viongozi waliopata kupitia hapa na wadau wengine waienzi shule hii,”anaeleza mwalimu mkuu wa shule ya msingi Mwisenge Redigunda Tairo.

Ukilitazama jengo ambalo aliishi Mwalimu aliyemfundisha Mwalimu Nyerere na viongozi wengine wakubwa katika Taifa hili utaungana nami katika makala hii kuona kuna umuhimu wa kumuenzi Mwalimu Nyerere kwa dhati na sio unafiki!.

Serikali haishindwi kujenga zile nyumba za walimu na kumalizi majengo chakavu ya shule ya msingi Mwisenge ambayo historia yake inatakiwa kuwa shule ya mfano maana hata wageni wanaofika Musoma uwa wanatamani kuona shule aliyosoma Baba wa Taifa lakini kwa hizi nyumba za walimu tunatia aibu.

Tukiachana na hilo la uchakavu wa baadhi ya majengo na nyumba za walimu,kwa mujibu wa Mwalimu Mkuu wa shule hiyo ambaye hakusita kuzungumzia changamoto za shule hiyo alielezea kuwepo na uhaba wa matundu ya vyoo na kusababisha usumbufu wa sehemu ya kujisaidia kwa wanafunzi wa shule hiyo!.

Matundu sita ya vyoo katika shule hii ndiyo yanayotumiwa na wanafunzi 808 wanaosoma kwenye shule hii na kuwafanya wanafunzi baadhi kwenda kwenye shule jirani kwa ajili ya kujisaidia hii si sawa ikiwa leo tunafanya kumbukumbu ya Baba wa Taifa aliyesoma kwenye shule hii.

Maji kwenye shule ya Mwisenge yamekatwa kwa zaidi ya miaka miwili kutokana na deni la miaka mingi ya nyuma na kuwafanya wanafunzi wa shule hii kutoka na maji nyumbani ama kufuata ziwani kwa ajili ya matumizi,lazima tuliangalie hili kama kweli tunamuenzi Mwalimu.

Leo tukifanya kumbukumbu ya miaka 14 ya kifo cha Hayati Baba wa Taifa hili,wanafunzi wa shule ya msingi Mwisenge bado wanakaa chini kutokana na upungufu wa madawati ili hali viongozi wengi licha Mwalimu wamesoma kwenye shule hii.

Hivi ni kweli tunapofanya kumbukumbu hii tunashindwa kuitembelea shule hii nakujua changamoto zake ili tusiwe na mambo mengi ya kuandika tukiwa tunamkumbuka muasisi wa taifa hili?.

Majibu ya swali hili ni rahisi tunajionyesha tupo karibu katika kumkumbuka Mwalimu kumbe ni unafiki huku tukiona wanafunzi wanaosoma kwenye shule aliyoma wakikosa sehemu ya kujisaidia,maji na wengine wakikaa chini.

Changamoto za shule zinapaswa kufanyiwa kazi mara baada ya siku hii kupita ili siku tutakapofanya kumbukumbu ya miaka 15 baada ya kifo cha Baba wa Taifa tusiwe wa kuandika haya ya wanafunzi wa shule aliyosoma kukosa mahala pa kujisaidia.

Najua inawezekana kama tutaamua na tukiacha unafiki wa kufanya kumbukumbu huku sehemu ya kumbukumbu zake zikiwa hazingaliwi na isitoshe tukaja kupata hesabu ya fedha nyingi ambazo zitatumika kutokana na siku hii.

Tumuenzi mwalimu kwa dhati na sio unafiki.        

Post a Comment