0


KATIKA kuonekana kutaka kuweka sawa Maadili ya Viongozi kwa mujibu wa Katiba,Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Musoma Mjini kimewavua Uanachama madiwani wawili wa viti maalum kwa utovu wa nidhamu na hivyo kupoteza sifa ya kuwa madiwani wanaotokana na Chama hicho. 
Akizungumza na Waandishi wa Habari Katibu Mwenezi wa Chadema Wilaya ya Musoma Meshack Ntongoni alisema baada ya kikao cha kamati tendaji kilichofanyika jana kiliazimia kuwavua uanachama madiwani wawili wa viti maalum kutokana na utovu wa nidhamu kwa mujibu wa ibara  ya 4.3 kutokana na mwenendo wao kuwa mbaya ndani ya Chama .



Aliwataja waliovuliwa uanachama ni Habiba Ally Zedy na Miriamu Daudi Chacha ambao wamekuwa wakionywa mara kwa mara kutokana na kutokubaliana na mambo ambayo yako ndani ya chama.

"Madiwani hawa tumekuwa tukiwaandikia barua mara kwa mara juu ya mwenendo wao wa utovu wa nidhamu ndani ya Chama na kwa Viongozi na wamekuwa wakikahidi hivyo kamati tendaji imeamua kuchukua hatua kwa mujibu wa Katiba.

"Hiki ni Chama ambacho viongozi wanapaswa kufuata utaratibu kwa mujibu wa katiba na hatutaweza kumvumilia kiongozi ama Mwanachama yeyote ambaye atakwenda kinyume na katiba yetu,"alisema Meshack.



Katibu mwenezi huyo pia aliwataja madiwani walioandikiwa barua ya mashitaka  ya kujibu ndani ya siku 14  kwa mujibu wa katiba  ya Chadema  ni pamoja na Meya wa Manispaa ya Musoma (CHADEMA) Alex Kisurura Diwani wa Kata ya Nyamatare ,Diwani wa Kata ya Kitaji Haile Siza Tarai ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango Miji  na Diwani wa Kata ya Kamunyonge Angela lima.


Alisema kamati tendaji ilichukua jukumu la kuwafuta uanachama kwa kufuata katiba ibara ya 5.(iv,iii) na kifungu namba 5.(iv)na vifungu vinne vingine ndani ya katiba ya Chama.

"Zipo kanuni nyingi sana zinazojitosheleza za madiwani hao kupata majibu yao ambayo yapo katika ibara ya 10.1 kifungu  cha i,iii,iv,v,viii,ix na x hivyo wasome wajirizishe,"aliongeza.

Alisema madiwani hao waliovuliwa uanachama wamekosa pia sifa ya kuwa madiwani kufutia taratibu,kanuni na sheria za katiba ya chama kuwa endapo mwanachama atapoteza sifa ya kuwa mwanachama pia anapoteza sifa za kuwa kiongozi katika ngazi yoyote ile.

Alisema madiwani hao walioandikiwa barua ya kutaka kujieleza wasipo fanya hivyo sheria itafanya kazi yake kwa kufuata vifungu vya katiba bila kuangali nafasi ya Diwani ndani ya Halimashauri.

Aidha alidai tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu uliopita wa kuchagua madiwani,wabunge na Rais ambapo walifanikiwa kuchukua halmashauri,hali ya chama hicho jimboni hapo ni tete kufuatia kutoelewana wao kwa wao hali inayopelekea chama kukosa mwelekeo.

"Tangu Chadema tumechukua jimbo tumekuwa na wakati mgumu sana hasa ya utomvu wa nidhamu,makundi,ukiukwaji wa katiba kwa ujumla,hali hii itatupeleka pabaya,hivyo tumeamua kuanza kuwadhibiti kwa kutumia makali ya katiba ili kukinusuru chama"alisema katibu huyo.

Hata hivyo madiwani hao waliopata dhoruba hiyo kila mmoja kwa nyakati walipokuwa wakihojiwa na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu walidai hawana taarifa za kikao hicho na wala hawajapewa barua za kuthibitisha maneno hayo.

"Mimi ninajijua ni Mwanachama wa Chadema na vilevile ni Diwani viti maalumu,kwa wanaosema maneno kuwa wamenivua uanachama ni propaganda zao za kisiasa tu"alisema Habiba.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Musoma Ahmed Sawa alisema hajapata barua kutoka Chadema juu ya hatua walizochukua kuhusu madiwani hao na kusema kuwa iwapo atapata taarifa hizo atasema namna utaratibu na kanuni zinavyoeleza.

Post a Comment