0
 
Chama cha walemavu Mkoa wa Mara kimeitaka serikali kuhakikisha inawashirikisha walemavu katika vikao muhimu vya kujadili maendeleo ngazi za vijiji,kata,wilaya na mkoa ili waweze kupata fursa ya kuwasilisha kero na mahitaji yao kwa serikali.

Mwenyekiti wa CHAWATA mkoa wa Mara Yohana Magai alitoa kauli hiyo mjini Musoma katika Mkutano wa watu wenye Ulemavu juu ya kujadili mapungufu ya utoaji wa haki za binadamu yaliyomo katika katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977.

Bw. Magai alisema licha ya marekebisho mbalimbali yaliyofanywa na Serikali katika katiba hiyo ya nchi, bado uwakilishi wa watu wenye ulemavu katika vikao vya maamuzi unaonekana ama kupuuzwa au kutopewa kipaumbele jambo ambalo ni kinyume na  mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu ambayo imeridhiwa kutekelezwa na serikali.

Alifafanua kwamba katika vikao vya kujadili na kutoa maamuzi juu ya mipango ya kimaendeleo kama vile kamati za maendeleo ngazi za vijiji(VDC),ngazi za kata(WDC),ngazi za wilaya(DDC) na mkoa (RCC) zinawakilishwa na taasisi mbalimbali vikiwemo vyama vya siasa lakini katika kamati hizo hakuna uwakilishi wa walemavu.

Kwa msingi huo alisema wakati Taifa likiwa katika mchakato wa kuandika katiba mpya itakayokidhi matakwa ya wananchi katika kujitawala, suala la haki mbalimbali za walemavu ukiwemo uwakilishi wa kundi hilo katika vikao vyenye maamuzi halina budi kupewa kipaumbele ili kuendana na sheria ya nchi ya watu wenye ulemavu Na 7 ya mwaka 2009.

Kwa upande mwingine Mwenyekiti huyo wa CHAWATA mkoani Mara bw. Yohana Magai aliwahimiza walemavu kuendelea kuibana Serikali katika utoaji wa haki za msingi kwa kundi hilo muhimu na kuachana na tabia ya kulalamika pembeni bila kuiambia serikali wajibu wake kwa walemavu.

Mkutano huo wa siku tatu juu ya kujadili katiba ya nchi ya mwaka 1977 na unaowashirikisha walemavu wenye matatizo ya viungo vya mwili toka wilaya za Rorya,Tarime,Serengeti,Bunda,Butiama na Musoma ulifunguliwa na katibu tawala wa wilaya ya Musoma bi Dora Makinga.

Awali akifungua Mkutano huo,Makinga alidai watu wanaoishi na Ulemavu wanayo nafasi ya kusikilizwa mawazo yao hivyo yale yote yatakayojadiliwa katika Mkutano huo wa siku tatu yanapaswa kusilizwa na kufanyiwa kazi ili kuwepo na ushirikishwaji wa pamoja katika kila jambo.

Post a Comment