0
MVUA kubwa iliyoambatana na upepo iliyonyesha wilayani Butiama mkoani Mara usiku wa kuamkia jana (juzi) imesababisha madhara makubwa kwa kubomoa nyumba 66 katika kijiji cha Mwibagi na kuwaacha Wananchi bila makazi.
 
Kufutia tukio hilo, Kamati ya Ulinzi na Usalama wilaya ya Butiama ilifanya ziara katika Kijiji hicho huku Mwenyekiti wa kamati hiyo Angelina Mabula akiwahimiza Wananchi wa Kijiji hicho kuwasaidia wananchi waliopata matatizo hayo wakati Serikali ikiendelea kufanya tathmini ya maafa hayo.
 
Akiwa katika kijiji hicho,Mabula alisema mvua zimeanza kwa kasi kubwa hivyo hatua madhubuti zinapaswa kuchukuliwa ili kuweza kukabiliana na athari nyingine kubwa ambazo zinaweza kutokea katika kipindi hiki cha mvua kwa kuimaliosha nyumba ambazo zinaonekana kuwa na hufa.
 
Mwenyekiti wa huyo wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wilaya ya Butiama pamoja na kupongeza hatua zilizochukuliwa za kusaidia wananchi waliopata tatizo la nyumba zao kubomoka alihimiza kudumishwa kwa ushirikiano huo wakati Serikali ikianza kufanya tathmini juu ana athari iliyotokea.
 
Alisema ni vyema kushirikiana kwa zile nyumba ambazo zinaweka kukarabatika ili watu wapate makazi kwa kusaidiana baina ya Wananchi pindi ambapo Serikali nayo inafanya jitihada za haraka kuhakikisha inatoa msaada wa haraka kwa wahathirika.
 
“Serikali ipo pamoja nanyi katika kipindi hiki kigumu ambacho mvua iliyoambatana na upepo mkali imeharibu makazi yenu wakati tunaendelea kufanya tathimini naomba ushirikiano uwepo hapa kijijini katika kupeana hifadhi.
 
“Hili ni janga ambalo lemekuja pasipo taarifa sasa kila mmoja alichukulie janga hili kama lake na kuweza kushirikiana katika kipindi hiki nasi tunatambua tatizo hili na tunalichukulia hatua za haraka,”alisema Mabula.
 
 Mmoja wa watu waliokumbwa na balaa la kukosa makazi katika kijiji hicho,Itembe Mtani aliiomba Serikali kufanya tathimini ya haraka ili kuweza kuwasaidia kupata makazi kwani familia nyingine ni duni na hazina uwezo wa kujenga nyumba hizo kwa haraka.
 
Alisema licha ya kukosa makazi mvua hizo pia ziliharibu chakula chote kilichokuwa kimehifadhiwa katika nyumba zao na kwa sasa familia hizo hazina chakula huku nyingine zikikosa pa kuishi nakuiomba Serikali kuwaangalia kwa jicho la huruma katika kipindi hiki.
 
Gazeti la Habari Leo lilishuhudia baadhi ya Wananchi wenye uwezo wakianza kujenga nyumba zao zilizobolewa huku wengine ni kama wamerudishwa tena kwenye dimbwi la umaskini baada ya kudai hawaoni pa kuanzia.

Post a Comment