0



TAASISI ya mfuko wa uwekezaji kiuchumi katika tarafa ya Nyanja(NEIT) Halimashauri ya Musoma mkoani Mara inatarajia kuwekeza zaidi ya sh bilioni 52 katika sekta mbalimbali kwenye Kata 17 za wilaya hiyo ikiwa ni mkakati wa kupunguza umaskini unaowakabili wananchi.
 
Mwenyekiti wa Taasisi hiyo ya (NEIT) Machumu alisema kwamba utekelezaji wa mkakati huo unatarajiwa kuzinduliwa rasmi mwezi January mwakani ambapo hadi hivi sasa vikundi 63 vya ujasiliamali na maendeleo vimekwisajiliwa katika taaasisi kama wanachama na kufungua akaunti zao benki.
 
Machumu alisema NEIT itasaidia kupunguza umasikini wa Wananchi wa Kata 17 za Wilaya ya Musoma katika sekta za Kilimo,Uvuvi,Ufugaji,Mazingira,Elimu na Afya ambapo miradi mikubwa kupitia sekta hizo itatekelezwa katika kipindi cha miaka mitano ya mradi unaoanza mwaka huu wa fedha wa 2013/14.
 
Alisema lengo la uwekezaji huo ni kuleta mageuzi ya kiuchumi kwa Wananchi walio wengi vijijini wanaoabiliwa na umaskini mkubwa ambapo baadhi ya miradi mikubwa iliyolengwa kutekelezwa katika mkakati huo ni mapinduzi ya kijani katika sekta ya kilimo kwa kushirikiana na Serikali katika mpango wake wa Kilimo kwanza kupitia ASDP na DADIPS.
 
Aliitaja miradi mingine itakayotekelezwa ni pamoja na uanzishwaji wa benki kata (SACCOS), benki ya Exim ambayo tayari imeshaonesha nia ya kujenga tawi katika Wilaya hiyo,boti za uvuvi za kisasa,ujenzi wa chuo cha mafunzo ya kilimo,chuo cha uuguzi na afya sanjari na ujenzi wa vituo 3 vya afya.
 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Askofu Alpha Modekaye Mashauri aliwataka Wananchi wa Wilaya hiyo kuanzisha kilimo cha kufa na kupona ili kuondokana na aibu ya kutegemea msaada wa chakula cha njaa toka serikalini kila mara kwa kuwa na chakula cha kutosha katika kaya zao.
 
Askofu Mashauri alisema licha ya Halmashauri hiyo kuongoza kila mwaka kwa baa la njaa kati ya halmashauri sita za mkoa wa Mara, nafasi bado ipo ya kuondokana na tatizo hilo kwa kufuata kanuni bora za kilimo,kuachana na uvivu wa kutofanya kazi sanjari na kutumia mbolea ya kupandia na kukuzia ya minjingu mazao.
 

Post a Comment