0
 Mkurugenzi wa Kituo cha Matangazo ya Televisheni cha Afrika (Africa TV) Bwana Muharami Iddiss akimkabidhi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Cheti maalum cha  Africa TV cha kuitumia ZBC – TV kurusha Vipindi vyake.
Makamu wa Pilio wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiwa katika picha ya pamoja na uongozi wa Africa TV ulioambatana na baadhi ya Viongozi wa Taasisi za Dini mara baada ya mazungumzo yao yalioyofanyika Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar. Kulia ya Balozi Seif ni Mkurugenzi wa Africa TV Bwana Muharami Idriss na Kushoto yake ni Mshauri wa Africa TV  Zanzibar Bwana Kassim Haidar Jabir.
*********************************************
Uongozi wa Kituo cha Matangazo ya Televisheni cha Afrika { Africa TV } wenye Makao Makuu yake Nchini Sudan umenasihiwa  kuendelea kufanya kazi zake  za kuelimisha jamii hasa umma wa Kiislamu kwa kuheshimu  maadili ya kazi zao ili kufanikisha vyema majukumu yake katika utaratibu uliojipangia.

Nasaha hizo zimetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar wakati akizungumza na Uongozi wa Afrika TV ulioambatana na baadhi ya Viongozi wa Taasisi za Dini ya Kiislamu ambao upo Zanzibar kujitambulisha rasmi ukijiandaa na utaratibu wa   kutangazwa matangazo yake kupitia Shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC - TV }. 

Balozi Seif alisema Vituo vya Habari  kama Afrika TV inayotoa matangazo ya Dini  vinaweza kusaidia kwa asilimia kubwa kuelimisha Jamii mfumo mzuri wa kufuatwa katika kulinda  Mila, Maadili na Taratibu za Kidini jambo ambalo husaidia kuiepusha  jamii kujiingiza katika matendo  maovu.
Alisema wapo baadhi ya masheikh na Walimu wa Dini hutumia fursa wanazozipata ndani ya vyombo vya Habari kwa kupotosha umma kujiingiza katika vitendo viovu ambavyo husababisha kutetereka kwa amani na utulivu wa Nchi.
 
Aliusisitiza Uongozi huo wa Afrika TV kuwa makini na wahadhiri wanaowatumia kwenye vipindi vyao ambao wakati mwengine  hutia ushawishi unaoleta uchochezi na hatimae kukosekana kwa utulivu wa jamii.
“ Tuwe na uhakika kwamba kinachotolewa na Afrika TV kinaelimisha vyema umma na kuwepuka ushawishi ambao unaweza kuleta fadhaa na kukosekana kwa utulivu wa moyo “. Alitahadharisha Balozi Seif.
“ Tunategemea sana kwamba Programu za Afrika TV zinatuelimisha vya kutosha na kupata faida iliyokusudiwa ya kueneza Daawa “. Alisisitiza Balozi Seif.
 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo kupitia Shirika la Utangazaji { ZBC TV } kwa kushirikiana na Vituo vyengine mbali mbali vya Matangazo vya kimataifa katika dhana na kuipatia Jamii Taaluma, Habari pamoja na kuipatia Elimu.
Mapema Mkurugenzi wa Afrika TV Bwana Muharami Idriss  alisema fikra za kuanzishwa kwa  Afrika TV iliibuka mnamo mwaka 2010 baada ya ufinyu wa  kukosekana kwa vyombo vya Habari vinavyopaswa  kuelimisha Umma wa Kiislamu ndani ya Bara la Afrika.
 
Bwana Muharami alisema Afrika TV ilianza rasmi  matangazo yake mwaka 2011 kwa kutumia Lugha Tano na kuongeza Lugha ya Kiswahili mwaka 2012 na baadaye lugha Tatu mwaka 2013.
Alieleza kwamba Uongozi wa Kituo hicho ulikuwa na azma ya kufungua Tawi la Studio yake  hapa Zanzibar  ili kuziongezea  nguvu zaidi zile za Dar es salaam na Mombasa Nchini Kenya ikiwapa fursa zaidi ya kutoa Taaluma  wahadhiri na Walimu wa hapa Zanzania.
 
Akitoa shukrani zake kwa Uongozi wa Kituo hicho cha Afrika TV Naibu Katibu wa Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Nauman Jongo alisisitiza umuhimu wa kufuatwa kwa taratibu za vyombo vya Habari ili kuepuka mapema cheche za ushawishi zinazoweza kuleta mfarakano ndani ya jamii  hapo baadaye.
Sheikh Jongo alisema baadhi ya vyombo vya Habari nchini vilipata fursa ya kutoa matangazo yake lakini vikajikuta whadhiri wake wakitumia zaidi ushawishi ulioonekana kuleta  mgongano wa kimawazo ndani ya mafundisho ya dini.
 
Lengo la Kituo cha Matangazo cha Afrika TV ni kutoa  Matangazo yake kwa zaidi ya  lugha 10 katika kipindi kifupi kijacho zitakazotoa huduma ya Taaluma katika mataifa mbali mbali Barani Afrika.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikutana na Mhariri Muandamizi wa Gazeti la Financial Report  { F.T. } lenye Makao Makuu yake London Nchini Uingereza Bwana Rohit Devan Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
 
Katika mazungunzo yao Bwana Rohit Devan anayesimamia miradi maalum kwenye Gazeti hilo ndani ya Kanda ya Afrika alisema Uongozi wa Gazeti hilo umeamua kuitangaza zaidi Zanzibar katika Nyanja za Kiutamaduni, Uwekezaji na Utalii.
 
Bwana Rohit Devan lisema wahadhiri, Wahariri na hata vyombo vingi vya Habari vya Kimataifa zimekuwa vikiitangaza  Zanzibar hasa zaidi katika eneo la Kisiasa na  Kihistoria.
 
“ Ukifanya utafiti wa haraka haraka unakuta waandishi wengi wa Kimataifa wameitangaza sana Zanzibar katika nyaja ya Kisiasa wakati Visiwa hivi vina rasilmali nyingi za Uwekezaji hasa katika sekta ya Utalii, biashara na Utamaduni “. Alifafanua Bwana Rohit Devan.
 
Mhariri huyo muandamizi wa Gazeti ya Financial Report alielezea matumaini yake kwamba kwa kupitia Gazeti hilo Zanzibar itajiuza vyema Kimataifa kwa vile limekuwa likichapishwa kwenye machapisho manne kila siku  katika vituo vya Miji ya Paris, London, Washington na Monako.
 
Naye kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliupongeza  Uongozi wa Gazeti hilo kwa uwamuzi wake wa kutaka kuitangaza Zanzibar Kimataifa katika Nyanja za Uwekezaj.
 
Balozi Seif alisema hatua hiyo itaipa Zanzibar muelekeo mzuri wa kufahamika zaidi katika Nyanja za Kimataifa katika suala la uwekezaji ambapo tayari Sekta ya Utalii imeshapewa msukumo zaidi katika kuongeza nguvu za Uchumi wa Zanzibar.
 
Aliuomba Uongozi wa Gazeti hilo la Financia Report  kuwa huru katika kuwasiliana na Taasisi na makampuni ya uwekezaji yaliyopo Nchini ili yapate fursa ya kujitangaza kupitia Gazeti hilo la Kimataifa.
 
KWA HISANI YA SUFIANIMAFOTOBLOG

Post a Comment