0
 

MBUNGE  wa  jimbo la Tarime  ametumia kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kugharimia  vitabu katika  shule mbalimbali za Sekondari katika jimbo hilo,lengo likiwa ni kuinua  kiwango  cha elimu na kufanya wilaya  hiyo kuwa na  amani na  kuwa  kimbilio la watu katika Nyanja mbalimbali za kiuchumi.
 
Akizungumza  na  waandishi  wa  habari,mbunge  huyo  Nyambari  chacha Nyangwine,alisema  kuwa  baada  ya  kuingia  madarakani  mwaka  2010  alikumbana  na  changamoto nyingi  zinazoikabili  sekta  ya  elimu  hatua  ambayo ilimfanya  kuchukua  hatua  za haraka  za kuchangia vitabu  hivyo  katika  shule  za  Sekondari ikiwa ni sehemu ya kutatua  changamoto hizo.
 
Alisema  kuwa wakati anachaguliwa  kuwa  mbunge  wa Tarime, wilaya  hiyo  ilikuwa  inatakabiliwa  na  tatizo kubwa  la  ukosefu  wa  amani  ya  kudumu huku akiwa na  shule 18 za  sekondari  lakini  kwa  juhudi zake,madiwani  na  halmashauri  wameweza kujenga  shule  hadi  kufikia  38 sasa hatua  ambayo  imefanya  wilaya  ya Tarime kupata  mabadiliko  makubwa  kimaendeleo.
 
“Wakati nachaguliwa  kulikuwa  na shule 18 za sekondari na zikiwa na  changamoto  kubwa nikaamua kuanza na tatizo la vitabu vya kujifunzia  na  kufundishia  na  hadi sasa  nimechangia  vitabu  vya  zaidi  ya  bilioni  moja huku  tukiwa  tumejenga  shule  za sekondari 20 kutoka 18  zilizokuwepo”alisema na kuongeza.
 
“Watu  wanashangaa  kuona  Tarime  leo  ni  wilaya inayokalika  kwa  kuwa  na  amani  ya  kudumu  huku ikipaa  kimaendeleo,mafanikio yote haya  yametokana na elimu”aliongeza mbunge huyo.
 
 
Alisema  kuwa amani hiyo ya kudumu kwa kiasi kikubwa pia imechangiwa  na  juhudi  zake  za  kukemea  baadhi  ya  watu  waliotaka  kuongoza  wilaya  hiyo  kwa kuwagawa  wazee  wa mila  ili  waweze kupata nafasi  za  kisiasa  kwa  kutumia  koo  watokazo.
 
“Tena  wanasiasa  hao  “uchwara”  wakiwemo  kutoka katika  chama  changu  wanakwenda  kushawishi  wazee wakisema  mimi  sitagombea  tena ubunge mwaka kesho,sasa nawaambia  nitagombea  na nitashinda kupita wakati ule,wasivuruge amani kwa kutaka kuchaguliwa”alisema na kuongeza.
 
“Tarime  ilikuwa  ni  wilaya  ya mfano wa mapigano  ya koo nchini,wakina  mama,vijana   walipoteza maisha,watu  walishindwa  kufanya  shughuli  za uzalishaji mali kama kilimo,kuzikana,kutembelea  hata kufikia  hatua ya kubaguana  kutokana  tu na uchu wa madaraka  uliofanya  baadhi  ya  wazee  wa mila kutumika  vibaya  kwa kusaidia  wanasiasa…hali hii  ilinitisha  sana  na nikasema  wakati  ule  wa  sherehe  ya kuwashukuru  wapiga  kura  kuwa ningependa  niongoze  Tarime  moja  na  leo ninyi mnashuhudia  Tarime  ni moja”alisema.
 
 
Hata  hivyo  alisema  baadhi  ya  wanasiasa  hadi  sasa hawapendi  hali  hiyo,wamekuwa  wakitumia  pesa kuwashawishi  hata  baadhi ya  viongozi   wa  mila kuungwa  mkono kwa  kutumia  koo  zao  kitu  ambacho  alisema kinaweza kuvuruga amani iliyopo na  kutosaidia  kabisa maendeleo  ya  wananchi   wa  Tarime.
 
Alisema hivi sasa ameanza kusimamia  ujenzi  wa chuo  cha ufundi   VETA  kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa vijana wanahitimu  elimu  ya darasa la saba  na kumaliza kidato cha nne  wanajiunga na mafunzo ya ufundi  ili kuwawezesha kujiajiri  wenyewe katika kukabiliana na tatizo kubwa la ajira kwa vijana.
 
Mbunge huyo wa jimbo la Tarime,ametumia nafasi hiyo kuutaka uongozi wa mgodi wa North Mara kutekeleza mara moja ahadi zake  kwa vijiji vinavyozunguka mgodi huo ikiwa ni pamoja na kulipa fidia ya  ardhi katika maeneo hayo ili kupunguza migogoro ambayo imekuwa ikisababisha kuteteleka kwa amani katika eneo hilo.
 
“Niliwahi kutoa kauli  ya  kufanya maandamano  ya kuwatoa  wawekezaji hao kwa kutumia nguvu  ya umma ili  kushinikiza  mgodi  kutekeleza  ahadi  zake,tulisitisha baada  ya  kutueleza  kuwa  wangetekeleza  ahadi  hizo na ulipaji  wa fidia  lakini  hadi  sasa hawajatekeleza”alisema  Nyangwine.
 
Kwa sababu hiyo aliutaka uongozi wa mgodi huo kutekeleza ahadi  hizo kabla ya mwezi desemba la sivyo atalazimika kutumia nguvu ya umma kushinikiza malipo hayo hata  kama nguvu hiyo  inaweza  kusababisha maafa katika eneo hilo ili kuwatendea haki wananchi hao ambao alisema  pamoja na kuzungukwa na madini lakini wamekuwa wakiishi katika timbwi kubwa la umasikini.
 
Mbunge  Nyangwine  aliongeza  kwa  kuitaka  serikali kuwatendea haki  wananchi  wanaozunguka migodi  za dhahabu ili  waweze  kunufaika  na  rasimali  hizo  badala ya kuwaona  wananchi hao kama  wahalifu huku wakiwakumbatia  wawekezaji pekee hatua  ambayo alisema  imekuwa ikichangia  migogoro  mingi katika maeneo hayo.
 

Post a Comment