0


MAKAMU wa Rais,Dkt.Mohamed Gharib Bilal,amewasili mjini Musoma kuungana na waumini wa dini ya kislamu katika swala ya sikukuu ya Idd al Hajj inayofanyika kitaifa mkoani Mara siku ya kesho.

Baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa Musoma,alikwenda kusaini kitabu chawageni kwenye ofisi ya mkuu wa mkoa wa Mara na kasha kuelekea  kwenye ofisi za Baraza la Waislamu mkoa wa Mara(Bakwata) na kukutana na viongozi wa dini ya kiislamu.

Akizungumzia na BINDA NEWS kuhusiana na maandalizi,Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya waislamu mkoa wa Mara,Said Gantala,alisema maandalizi kuhusiana na ibada hiyo ambayo huadhimishwa duniani kote baada ya kumalizika kwa Hijja yamekwisha kukamilika yakiwemo maandalizi ya harambee hiyo.


Amesema baada ya kumalizika kwa swala itakayoswaliwa kwenye viwanja vya shule ya msingi mkendo kuanzia saa 2 kamili,kuanzia  mchana kutafanyika Baraza la Idd litakalofanyika kwenye ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania tawi la Mara ambapo pamoja na mambo mengine yatakayozungumzwa kutafanyika harambee kwaajili ya kuchangia ujenzi wa msikiti wa Ijumaa wa mkoa wa Mara.




Gantala amesema harambee hiyo inafanyika kutokana na Msikiti ambao umekuwa ukitumika kwa muda mrefu kama Msikiti mkubwa unaotumiwa na watu wengi kuwa na nafasi ndogo pamoja na kuchaka kwa miundombinu yake.

Amesema katika kuweza kufanikisha ujenzi wa msikiti huo wa kisasa,kiasi cha shilingi bilioni 1.5 zinahitajika na wametoa mialiko ya kushiriki kwa waumini wote wa dini ya dini pamoja na viongozi mbalimbali ili kuweza kufanikisha shughuli hiyo.

Amesema ujenzi wa msikiti ni sadaka yenye kudumu na malipo yake yatapatikana siku ya hukumu mbele ya Mwenyezi Mungu hivyo kutoa wito kwa kila mmoja kuona umuhimu wa kushiriki kwenye ujenzi wa nyumba ya ibada.

Idd al Hajj, husheherekewa kama kumbukumbu ya sadaka ya  Ibrahimu ambaye kufuatana na taarifa za Qurani alikuwa tayari ya kumchinja mwanawe kama sadaka kwa Mungu lakini Mungu alimzuia asimchinje akampatia kondoo badala yake, Qurani  sura al-Hajj aya 37.


Post a Comment