0
 

FAZEL  JANJA

Musoma.

MOJA ya malengo ya serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Pombe Magufuli, ni kupambana na rushwa ambayo ni adui wa haki na kikwazo kikubwa cha maendeleo.
 


Mkuu wa Takukuru mkoa wa Mara,Holle Makungu
 
 
Hata wakati akilifungua Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mjini Dodoma Novemba 20, 2015; kwa kuonesha msisitizo juu ya dhamira yake hiyo, Rais alitoa ahadi ya kuanzisha Mahakama Maalumu ya kushughulika  na makosa ya Rushwa na Ufisadi.
 
“Katika kushughulikia tatizo hili nimeahidi kuunda mahakama ya rushwa na ufisadi, ni matumaini yangu vyombo husika katika jambo hili havitanikwamisha…” ilisema sehemu ya hotuba ya Dk. Magufuli.
 
Katika hotuba yake hiyo rais anaoneshwa kukerwa na vitendo vya rushwa na ufisadi vilivyoshamiri nchini na kwamba vinawanyima haki wananchi na kuitia serikali hasara ya mabilioni ya fedha; huku akifafanua kuwa fedha hizo zinazopotea kwa njia ya rushwa zingeweza kutumika kugharamia miradi mbalimbali ya maendeleo.
 
Magufuli anakwenda mbali na kunukuu maneno ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere aliyoyatoa Mei, 1960 wakati akilihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano. “Rushwa haina budi kushughulikiwa bila huruma kwa sababu naamini wakati wa amani, rushwa na ufisadi ni adui mkubwa kwa ustawi wa watu kuliko vita.”
 
Rais anasisitiza kuwa hayo ni maneno makali ya mtu na kiongozi aliyeichukia na kuikemea rushwa katika maisha yake yote ya uongozi; anasema kauli hiyo ya Mwalimu inatahadharisha hatma ya taifa letu endapo tutaendelea kuendekeza rushwa na ufisadi.
 
Aidha katika hotuba yake hiyo rais anatanabaisha wazi kuwa chuki ya wananchi kwa sasa ni dhidi ya vitendo vya rushwa na ufisadi na kwamba ni dhahiri kuwa wamechoka kabisa na hawako tayari (tena) kuendelea kuivumilia serikali itakayoonea haya rushwa na kulea mafisadi.
 
Ndiyo maana Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, (TAKUKURU) mkoani Mara, kwa kuitikia na kuzingatia agizo hilo la Rais Dk. John Pombe Magufuli la kutomuangusha katika kutimiza malengo yake hayo; imepanga mikakati madhubuti kuhakikisha inakwenda sambamba na kasi ya serikali yake chini ya kauli mbiu ya ‘Hapa Kazi Tu’.
 
Akizungumza hivi karibuni na vyombo vya habari mkoani hapa, Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Mara Holle Makungu anataja sehemu ya mikakati hiyo sambamba na taarifa ya miezi mitatu (Januari – Machi, 2016) ya utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo.
 
Anasema mikakati na majukumu hayo ni kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya mwaka 2007 na sheria zinazohusiana, kama ile ya kuzuia utakatishaji fedha namba 12 ya 2006 na ile ya mali zinazopatikana kwa njia za kihalifu (the Proceed of Crime Act, Cap 256) ya 1991.
 
Makungu anaitaja mikakati hiyo pamoja na mambo mengine; kuwa ni kuhakikisha kwamba watumishi wote wa umma wanaotumia vibaya nyadhifa zao  kwa vitendo vya rushwa na ufisadi, wanachukuliwa hatua stahiki ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi kupitia waajiri wao na kufikishwa mahakamani mara moja.
 
Mbinu nyingine ni kufuatilia fedha za umma kwenye halimashauri kama zinafanya kazi stahiki na iliyokusudiwa; kuendelea kutoa elimu kwa madiwani, wakuu wa idara na wananchi kwa ujumla juu ya namna mbalimbali za kuzuia na kupambana na rushwa ikiwa ni pamoja na kuvishauri vyama vya siasa kuwanyang’anya kadi wabunge ama madiwani wanaotumia vibaya nyadhifa za kisiasa, kama kinga kwao dhidi ya tuhuma za makosa ya rushwa na ufisadi.
 
Aidha Makungu anafafanua kuwa ofisi yake imekuwa ikitekeleza majukumu yake ya kila siku kupitia utaratibu wa aina tatu ambao ni pamoja na kufanya uchunguzi, kutoa elimu kwa umma sanjari na udhibiti.
 
Katika kipindi cha miezi mitatu dawati la elimu kwa umma limeimarisha kwa njia ya elimu Klabu za Wapinga Rushwa 55 ndani ya mkoa, ili kuwaandaa vijana na wananchi katika mapambano dhidi ya rushwa, ambapo semina 31 zimefanyika; mikutano ya hadhara 13 ikiwa ni pamoja na kuchapisha vijalida, Makala, maonesho na vipindi kadhaa vya redio na machapisho mengine 2,888 yenye ujumbe mbalimbali wa vita dhidi ya rushwa yaliyowafikia watu zaidi ya 11,000.
 
Aidha kwa upande wa udhibiti Makungu anasema katika maeneo mbalimbali walikofanya udhibiti, dhibiti 7 zimefanyika katika Idara ya Afya, Elimu, Maji na Ardhi.
 
Akizungumzia kwa upande wa ukaguzi wa miradi mbalimbali, mkuu huyo wa Takukuru anasema kuwa kwa kipindi cha miezi hiyo mitatu, wamekagua miradi zaidi ya 20 ya maendeleo iliyokuwa ikiendelea na iliyokamilika hapa mkoani; wakifuatilia kwa makini kabisa thamani ya pesa kulinganisha na ubora wa viwango vya utekelezaji wa mradi husika (value for money).
 
Anasema ni kupitia utaratibu huo pamoja na mambo mengine, wamebaini kuwa miradi mingi imekuwa ikifunguliwa kila mwaka kupitia mbio za mwenge lakini kwa sababu ya rushwa, mingi kati yake ama imeshindwa kukamilika kabisa, ama imekamilika katika viwango duni licha ya kuwepo kwa wataalamu na washauri wa kitaalamu katika halimashauri zetu.
 
“Tumebaini baadhi ya makandarasi kulipwa fedha zote hata kabla ya mradi kukamilika…mfano ujenzi wa nyumba za walimu Shule ya Sekondari Kyabakari, fedha zote 125,000,000/= zimekwishalipwa kwa mkandarasi wakati jiko katika moja ya nyumba hizo haijakamilika…tunamtaka kandarasi kukamilisha kazi hiyo ndani ya mwezi mmoja la sivyo sheria ichukue mkondo wake.” Anasema Makungu.
 
Mkuu huyo wa Takukuru mkoani Mara anasema ndiyo sababu ofisi yake katika kipindi cha miezi mitatu tu imepokea taarifa/malalamiko 179 kutoka vyanzo mbalimbali ambapo kati yake 150 yamefunguliwa majalada ya uchunguzi wa awali, 7 yamefanyiwa udhibiti, moja limehamishiwa idara nyingine huku walalamikaji 21 wakipewa ushauri wa kisheria.
 
Aidha anasema malalamiko hayo yaliyopokelewa mengi yanahusu miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ile ya TASAF III pamoja na mishahara hewa (wahusika wakiwa ni Tamisemi), ambapo malalamiko mengine yanahusu mahakama, Jeshi la Polisi, NHIF, TRA, TFDA, Uhamiaji, Afya (hospitali ya mkoa na zahanati), Muwasa na Tanesco.
 
“Hadi sasa kesi 42 zinaendelea katika mahakama mbalimbali za wilaya na mkoa wa Mara huku kesi tano zikiwa tayari zimekwishatolewa hukumu kwa mujibu wa sheria za nchi.” Anasema Makungu.
 
Akijibu swali kutoka kwa mwandishi wa Makala hii kuhusiana na madai kuwa taasisi hiyo imekuwa ikiwakamata watuhumiwa ‘vidagaa’ wa rushwa na kuwagwaya ‘mapapa’ Makungu anakanusha vikali madai hayo.
 
“mimi natekeleza majukumu yangu katika ngazi ya mkoa…sijui ni vigogo gani hao unaotaka niwakamate…nimemfikisha mahakamani Katibu Tawala wa Mkoa (RAS), DED wa Serengeti na hata Hakimu Mwandamizi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma…kigogo gani mwingine unayemtaka?” Anahoji.
 
Makungu anawataka wananchi wote kushirikiana na Takukuru kwa kutoa taarifa sahihi na kwa wakati juu ya jambo lolote lenye harufu ya rushwa na kwamba Sheria ya Takukuru Na. 51 na 52 inamlinda mtoa taarifa.
                                             
 0655 872873,  0784 872873.
                        
 
 
 
 
 
 
 

Post a Comment