0

DIWANI wa Kata ya Kitaji katika manispaa ya Musoma, Frenk Wabare, ameliomba baraza la madiwani la halmashauri hiyo kuacha kuongeza ushuru wa asilimia 40 kwa wafanyabiashara wa soko kuu la Musoma kwa kuwa wanafanya biashara kwenye mazingira magumu.
Akizungumza kwenye kikao cha baraza la madiwani cha kupitisa rasimu ya bajeti ya halmasauri hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2018 hadi 2019, amesema mazingira ya soko sio mazuri ikiwemo kushindwa kufanya biashara pale mvua inapokuwa inanyesha kutokana na kutokuwa na miundombinu mizuri ya kutoa maji hivyo sio vyema kuwaongezea ushuru wakati hawajafanyiwa marekebisho. 
Amesema amekuwa akikutana na wakati mgumu anapotembelea soko hilo ambalo lipo kwenye Kata yake kutokana na malalamiko ya wafanyabishara na halitakuwa jambo la busara kuwaongezea gharama za ushuru wakati mahitaji yao hayajatekelezwa.
Wabare alisema ni vyema kwanza yakatekelezwa yale ambayo wafanyabiashara hao wamekuwa wakiyalalamikia ndipo waweze kukaa nao chini kuona kama kutakuwa na sababu za kuwaongezea gharama za ushuru ambazo wanatakiwa kuzilipa.
Diwani huyo amesema nyakati za mvua maji yamekuwa yakijaa kwenye soko hilo na kuwafanya kushindwa kufanya biashara na kuwaomba madiwani kwa kuwa soko hilo linawahudumia wakazi wote wa manispaa ya Musoma ni vyema wakakubaliana na maombi yake ya kutoongeza gharama za ushuru
Aidha diwani huyo ameliomba baraza hilo kukubali kuhamisha fedha zilizotengwa kiasi cha shilingi milioni 20 kwenye bajeti ya mwaka 2018-2019 kwaajili ya ujenzi wa duka kubwa (super markert) kwenye bustani ya Malikia Elizaberth iliyopo eneo la stend ya zamani na kuzipeleka kwenye ukarabati wa soko pamoja na ujenzi wa nyumba ya kupumzika abiria.
“Naomba tusiwaongezee gharama za ushuru hawa wafanyakazi wetu kutokana na mazingira ya pale sokoni kutokuwa mazuri kwa sasa tujikite kwenye kuboresha baadae tutazungumza nao kama kuna sababu za kuongeza gharama za ushuru.
“Lakini nawaomba waheshimiwa madiwani tukubaliane na ombi langu zile fedha ambazo zimetengwa kwaajili ya ujenzi wa duka kubwa pale kwenye bustani ya malikia ziamishiwe kwenye ukarabati wa soko na jengo la abiria kupumzika pale kwenye stend yetu,”alisema Wabare.
Kupitia maombi ya diwani huyo, Meya wa manispaa ya Musoma, Patrick Gumbo, aliwahoji madiwani wa halmashauri hiyo kama wanakubaliana na maombi hayo na kukubali kwa pamoja kulidhia maombi ya diwani huyo ili kuondoa adha kwa wafanyabiashara wa soko kuu pamoja na wasafiri.









Post a Comment